Friday, April 20, 2012

Pinda kujiuzuru? Tusubiri!!

WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda, sasa yuko katika hatari ya kuondolewa madarakani kwa kupigiwa kura ya kutokuwa na imani naye kufuatia tuhuma nzito za ubadhirifu wa fedha za umma unaodaiwa kuwahusisha mawaziri watano wakiongozwa na Waziri wa Fedha Mustafa Mkulo.

Akiwasilisha majumuisho ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, mwenyekiti wa kamati hiyo, Zitto Kabwe, aliliambia Bunge kuwa kuanzia leo wataanza kukusanya saini za wabunge wenye nia ya kupiga kura hiyo na kwamba uamuzi wake utawasilishwa bungeni Jumatatu wiki ijayo.

Mwenyekiti huyo alisema ikiwa mawaziri hao ambao hata hivyo hakuwataja majina mmoja baada ya mwingine hawatakuwa wamejiuzulu wenyewe hadi kufikia siku hiyo, basi wabunge watamwondoa Pinda madarakani kwa kumpigia kura ya kutokuwa na imani naye.

Kwa hali hiyo, Zitto alisema kuwa itakuwa ni jukumu la mawaziri hao kabla ya Jumatatu wiki ijayo kuamua wenyewe kujiuzulu au kumwacha waziri mkuu atimuliwe.

Hatua hiyo ya Zitto ilitokana na hoja iliyokuwa imetolewa mapema na Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA), ambaye aliwataka wenyeviti wa kamati za Bunge wakati watakapokuwa wanajumuisha hoja zao kupendekeza kupiga kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu Pinda ikiwa mawaziri wake hawatakuwa wamejiuzulu wenyewe.

Lissu alisema wakati wa kupiga kelele umekwisha, na sasa wanachotakiwa ni kuchukua hatua, kwani mamlaka hiyo wanayo kwa mujibu wa Katiba.

“Waziri Mkuu wajibika kwa madudu ya serikali. Nitaomba wenyeviti wa kamati hizi wanapomalizia mjadala huu kupendekeza kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu kwa kujenga mfumo wa siasa wa udokozi. Tukifanya hivyo wananchi watatuamini. Ninyi chama tawala ndio mnaosababisha haya kama mtatumia wingi wenu sawasawa tutafanikiwa, sisi tupo wachache.

“Badala ya kupiga makofi, chukua hatua kwa uozo huu. Mkifanya hivyo mtaheshimika na msipofanya hivyo mtaingia kwenye vitabu vya historia,” alisema.

Alisema masuala ya ufisadi yamekuwa yakizungumzwa na zaidi ya miaka 10 sasa, lakini hawajawahi kuona serikali ikichukua hatua.

“Wakati kila mwaka CAG anatuletea taarifa za wizi, hatujawahi kuona serikali ikichukua hatua dhidi ya wahusika. Hatujawahi kuona mtendaji amechukuliwa hatua wala waziri kuwajibika katika hili. Watu wanapata kupata nafasi za uwaziri ili kuhujumu nchi,” alisema na kuongeza mfumo uliopo ni wa kulinda wezi.
http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=35063

No comments:

Post a Comment